Advertise here

Maandiko Yasemavyo Kuhusu Manabii na Mitume wa Kweli na Uongo

Maandiko Yasemavyo Kuhusu Manabii na Mitume wa Kweli na Uongo

Huduma ya mitume na manabii wa uongo na hasa ya kinabii, ilitabiriwa tangu enzi za Agano la Kale, kwamba itakuwepo duniani, na sasa ipo.
Kitabu cha Yeremia 14:14: "NDIPO BWANA AKANIAMBIA, HAO MANABII WANATABIRI UONGO KWA JINA LANGU MIMI, MIMI SIKUWATUMA, WALA SIKUWAAMURU, WALA SIKUSEMA NAO, WANAWAPENI UNABII WA MAONO YA UONGO, NA UAGUZI, NA MANENO YA UBATILI, NA HADAA YA MIOYO YAO".

Unabii huu wa mtumishi Yeremia ndio unatoa picha halisi ya jinsi MANABII NA MITUME WA UONGO WANAFANYA KAZI KWA KUTUMIA ROHO YA MAPEPO KUDANGANYA WATU na kujipatia kipato kupitia jina la Yesu.

Kati ya mambo ambayo Yesu alitahadharisha kuhusu nyakati za mwisho ni KUONGEZEKA kwa uvumi wa vita na manabii wa uongo. Maana yake ni kuwa YALIKUWEPO, ILA YATAONGEZEKA. Mathayo 7:15-16: "jihadharini na manabii wa uongo, Watu wanaowajia wamevaa mavazi ya kondoo, walakini kwa ndani ni mbwa mwitu wakali". Mathayo 24:11: "na manabii wa uongo watatokea na kuwadanganya wengi".

Kwa nini Yesu alitahadharisha ujio wa huduma hii kwa manabii wa uongo, na siyo wainjilisti, walimu au wachungaji wa uongo?
Hii ni kwa sababu HUDUMA YA KINABII NI HUDUMA INAYOHUSIANA NA MAFUNUO NA MAONO PIA.

Manabii wengi wanajitanabaisha kuongozwa na roho kuliko neno la Mungu. Kwa hiyo nabii ni mtumishi mwepesi sana kuweza kutumiwa au kudanganywa na shetani, kwa sababu baadhi, ndani yao hawana neno la Mungu la kutosha.
Kumbuka kuwa Neno la Mungu ni silaha ya kumshinda shetani na mitego yake. Ndiyo maana Yesu alipojaribiwa alimshinda shetani kwa Neno na si kwa sababu yupo rohoni sana.

Kwa hiyo, kukosa Neno la Mungu ndani ya baadhi yao kunamfanya shetani kuteka nyara fahamu zao na kuwaingiza rohoni kwa kuwaonesha vitu vya kiroho, wakidhani ni maono toka kwa Mungu.

Hivyo, Mungu anakumbusha waliookoka (waumini wa Yesu), kuzijaribu hizi roho za manabii, ili kujua kama zimetokana na Mungu, au shetani.

1Yohana 4:1 "wapenzi msiiamini kila roho, Bali zijaribuni hizo roho, kwamba zimetokana na Mungu, kwa maana manabii wa uongo wengi wametokea duniani".
Kumbuka pia kuwa shetani hujigeuza malaika wa nuru ili apate kuwadanganya watu.

DALILI ZA KUMTAMBUA NABII AU MTUME WA UONGO
Kitabu cha Kumbukumbu la Torati 18:20-22 kinasema:
20 Lakini nabii atakayenena neno kwa kujikinai kwa jina langu, ambalo sikumwagiza kulinena, au atakayenena katika jina la miungu mingine, nabii yule atakufa. 21 Nawe ukisema moyoni mwako, Tutajuaje neno asilolinena BWANA? 22 Atakaponena nabii kwa jina la BWANA, lisifuate jambo lile wala kutimia, hilo ndilo neno asilolinena BWANA; kwa kujikinai amelinena huyo nabii, usimwogope.

1. Kuhubiri zaidi injili ya miujiza na kubariki watu kuliko injili ya kutafuta ufalme wa mbinguni
Ukiona mtumishi anapenda kuhamasisha watu kuja kanisani kwake kwa ajili ya kupata miujiza, na siyo kuja kujifunza Neno ili watu wapate kumjua Mungu, huyo ni wa kutilia mashaka. Yesu alisema hivi: (Mathayo 6:33) "utafuteni kwanza ufalme wa Mungu na haki yake, na hayo mengine mtazidishiwa".
Kipaumbele cha injili ya Yesu hakikuwa muujiza, bali ilikuwa watu wautafute kwanza ufalme wa mbinguni na haki yake, na mengine atawazidishia. Kwa hiyo, miujiza ilikuwa sehemu tu ya matokeo ya injili hiyo, siyo kipaumbele.

2. Kutoonya watu kuhusu kuacha kutenda dhambi, kwa kuhofia washirika kukimbia
Ukimuona mtumishi hataki kuwaonya watu kuhusu kuacha dhambi, ujue huyo ni nabii wa uongo.
Maandiko yanasema hivi "wale wadumuo kutenda dhambi uwakemee mbele ya watu wote, ili na wengine waogope" (1Timotheo 5:20). Mahali pengine anasema hivi, "Nena maneno haya, onya na karipia kwa mamlaka yote, asikudharau mtu (Tito 2:15).

3. Anaikanyaga na kuitupilia mbali huduma ya ubatizo wa maji mengi na ya roho mtakatifu
Ukiona mtumishi hataki kuwabatiza watu kwa maji mengi, au kuwafundisha watu habari za ujazo wa roho mtakatifu, huyo ni wa kumkimbia, ni nabii wa uongo, atakupoteza.

Yesu alisema hivi: "Amini, Amin, nakuambia mtu asipozaliwa kwa maji na kwa roho hawezi kuingia ufalme wa Mungu" (Yohana 3:5). Kuhusu ubatizo, ni muhimu kufahamu kuwa Yohana mbatizaji alimbatiza Yesu katika maji tele (Mathayo 3:13-17). Yesu Kristo alibatizwa katika mto Yordani kwa sababu huko kulikuwa na maji tele.

Chimbuko la ubatizo wa maji mengi
UBATIZO
kwa kugha ya Kiingereza, baptism, maana yake Kiebrania ni "kuzamisha kabisa chini ya". Hivyo, ubatizo wa maji mengi maana yake ni kuzamisha kabisa chini ya maji. Ndilo chimbuko la ubatizo wa maji mengi. Tafsiri yake ilikuwa ni aina ya kufa, kuzikwa na kufufuka kwa Kristo (Warumi 6:3-5). Hivyo, unapozamishwa majini, tafsiri yake ni kuwa unakufa na Yesu na kufufuka na Yesu. Maana yake ni kwamba ya kale yamepita, tazama, umekuwa kiumbe kipya ndani ya Kristo.
Hiyo ndiyo sababu ya kuzamisha wakati wa ubatizo wa maji mengi. Ni kudhihirisha mtu wa zamani kuzikwa, na mtu mpya kufufuliwa katika uzima mpya.

Matumizi ya maji kidogo kwa ubatizo, kama ilivyoainishwa kwenye Matendo 2:41, Matendo 16:15 na Matendo 16:33, yalikuwa ni kwa mazingira maalum ya papo kwa papo tu. Hiyo ikiwa ni pamoja na kwa minajili ya mazingira ya mgonjwa mahututi, nk.

4. Anajali maslahi ya pesa kanisani kuliko utu

Mifano ni kama vile: (i) huwezi kuonana naye hadi ulipe pesa ya kumuona, (ii) huwezi kuombewa hadi utoe pesa, (iii) huwezi kupata cheo kanisani kwake hadi uwe na pesa.
Kitabu cha 2Petro 2:2-3 kinasema:
2 Na wengi watafuata ufisadi wao; na kwa hao njia ya kweli itatukanwa. 3 Na katika kutamani watajipatia faida kwenu kwa maneno yaliyotungwa; ambao hukumu yao tangu zamani haikawii, wala uvunjifu wao hausinzii. Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi " mmepewa bure kazi ya kuponya watu, toeni bure msiombe pesa, wala dhahabu." (Mathayo 10:8-9).

5. Hawapendi kuwafundisha washirika kweli ya neno la Mungu ili wakue kiroho na wamjue Mungu vizuri
Wanahofia kupoteza nafasi ya kuwatawala na kuwamiliki kwa sababu watakuwa wanaojitambua kwa kulijua Neno.
Wanataka kuendelea kuwakandamiza, kuwaibia pesa na kuwaonea kwa sababu ya ujinga wao wa kiroho.
Yohana 8:31-32 "mtaifahamu kweli nayo kweli itawaweka huru". Kulijua Neno la Mungu vizuri kunakutoa katika gereza la utumwa wa kiroho.

Mtu akishamwamini Yesu, kuwa Bwana na mwokozi ya maisha yake, anafanyika kiumbe kipya; ya kale yanapita, na tazama, yanakuwa mapya (2Korintho 5:17).

Aidha, anapata uwezo wa kutambua manabii na mitume wa kweli na uongo.

Kupata maarifa ya kiroho kama yaliyomo humu, ni kujiweka kwenye nafasi nzuri ya kujinasua kutoka kwenye mitego ya manabii wa uongo.
 
Hoja ni ubatizo wa maji, lakini issue ya maji mengi au machache haina mashiko,ubatizo una maana ya kusafishwa, kuoshwa dhambi

Ezekieli 36:25
[25]Nami nitawanyunyizia maji safi, nanyi mtakuwa safi; nitawatakaseni na uchafu wenu wote, na vinyago vyenu vyote.
 
Maeneo mengine umezungumza sahihi
Tukumbuke kuwa Yesu alibatizwa mtoni kwenye maji mengi. Kama ni kutumia hata maji kidogo tu kumwosha, hiyo mbona ilikuwa kazi nyepesi tu, kwani maji hayakosekani. Lengo lilikuwa ni kudhihirisha tendo la kuzama (kufa), yaani kuzika dhambi, na kuibuka juu (kuwa mshindi/shujaa), yaani kuanza upya. Ni kuzingatia dhana/maana iliyo ndani ya kitendo chenyewe, na siyo suala la kuoshwa kama kuoshwa kirahisi tu. Ni katika muktadha wa kuzika na kuanza upya. Katika kuoshwa tu, hakuna dhana ya kuzika ndani yake.
 
Tukumbuke kuwa Yesu alibatizwa mtoni kwenye maji mengi. Kama ni kutumia hata maji kidogo tu kumwosha, hiyo mbona ilikuwa kazi nyepesi tu, kwani maji hayakosekani. Lengo lilikuwa ni kudhihirisha tendo la kuzama (kufa), yaani kuzika dhambi, na kuibuka juu (kuwa mshindi/shujaa), yaani kuanza upya. Ni kuzingatia dhana/maana iliyo ndani ya kitendo chenyewe, na siyo suala la kuoshwa kama kuoshwa kirahisi tu. Ni katika muktadha wa kuzika na kuanza upya. Katika kuoshwa tu, hakuna dhana ya kuzika ndani yake.

Kuhusu Ezekieli 36:25

Hiki kifungu kinaonesha uamuzi au neema ya Mungu mwenyewe. Na hakuna tendo ambalo Mungu atafanya physically. Ni neema tu kwa watu wake. Neema hiyo ndiyo imeandikwa kuwa ni kunyunyizia maji kiroho, lakini kiuhalisia hakuna maji yatachotwa na kunyunyizia.

Kitendo cha maji mengi ni uamuzi wa mtu mwenyewe kutaka kusafishwa. Katika kufanyiwa hivyo, huandamana na matamko ya kukiri na kutubu kwa mtu mwenyewe. Hii haiji yenyewe, bali ni baada ya mtu mwenyewe kuamua kubadilika. Hii ni tofauti na ile ya kunyunyiziwa maji na Mungu mwenyewe, kwa uamuzi wake na kwa neema yake mwenyewe.
Kwa hiyo, kifungu hiki hakijielekezi kwa uamuzi wa mtu kuachana na dhambi, bali ni uamuzi na neema tu ya Mungu mwenyewe.
 
Back
Top