Advertise here

Tofauti ya Congo Kinshasa (Zaire) na Congo Brazzaville

Kasomi

JT Founder

Kwa nini nchi mbili za Afrika zinaitwa Congo?

Watu wengi barani Afrika na ulimwenguni kote mara nyingi huchanganya nchi mbili za Kiafrika - Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na Jamhuri ya Congo. Hapa kuna mwongozo rahisi.

Watu wengi duniani wanashangaa kwa nini kuna Congo mbili - zote barani Afrika - Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na Jamhuri ya Congo.
Screenshot_20251204-002310~2.jpg

Picha ni Bendera za Nchi hizi mbili: kulia ni Bendera ya Congo Brazzaville na Kushoto ni Bendera ya Congo Kinshasa
Nchi hizo mbili ni majirani katika Afrika ya kati.

Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, nchi ya pili kwa ukubwa barani Afrika, ina ukubwa wa kilomita za mraba milioni 2.3 na ina wakazi wapatao milioni 110.

Jamhuri ya Congo ina ukubwa wa kilomita za mraba 342,000 na idadi ya watu milioni 5.7.

Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo au DRC, ina Kinshasa kama mji mkuu wake wakati Jamhuri ya Congo ina Brazzaville kama mji mkuu wake.

Kwa hiyo, ili kuepuka utata, nchi hizo mbili mara nyingi hutofautishwa na majina ya miji yao mikuu - Congo Kinshasa na Congo Brazzaville.

Rais wa sasa wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (Congo-Kinshasa) ni Felix Tshisekedi wakati rais wa sasa wa Jamhuri ya Congo (Congo-Brazzaville) ni Denis Sassou Nguesso.

Ushawishi wa kikoloni

Kabla ya ukoloni, Congo hizo mbili zilikuwa sehemu ya Ufalme mmoja - Ufalme wa Congo - ambao pia ulijumuisha Angola ya sasa.

Nchi zote mbili sio tu zina jina sawa, watu wao bado wanazungumza lugha moja - Kilingala na Kikongo.

Pia wote wawili wana Kifaransa kama lugha yao rasmi kwa sababu ya historia yao ya kikoloni.

Congo-Brazzaville ilitawaliwa na Ufaransa. Ingawa, Congo Kinshasa kwa upande mwingine ilitawaliwa na Ubelgiji, Wabelgiji pia walikuwa wakizungumza Kifaransa kama lugha rasmi.

Mataifa ya Ulaya yalifyonza rasilimali za Congo hizo mbili. Nchi hizo mbili zinazunguka Mto Congo na zimejaliwa kuwa na maliasili kubwa zikiwemo dhahabu, kobalti na shaba.

Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC)

Ni muhimu kutaja kwamba mipaka ya kisasa katika Afrika ilichorwa wakati wa kugawanyika kwa bara wakati nchi za Ulaya zilijitengea maeneo katika Mkutano wa Berlin wa 1884-1885.

Mfalme Leopold wa Pili wa Ubelgiji aliushawishi mkutano huo kumruhusu kudhibiti eneo la Congo, kutokana na kile kinachoitwa ‘juhudi zake za kibinadamu’ huko.

Kisha akaliita Jimbo Huru la Congo - ambalo ni Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ya sasa.

Hata hivyo, ukatili mwingi ulifanyika wakati wa utawala wake ikiwa ni pamoja na mauaji, mateso na njaa.

Watu wa Congo walilazimishwa kufanya kazi kwa rasilimali kama vile mpira na pembe za ndovu ili Leopold aweze kujitajirisha.

Makadirio yanatofautiana, lakini zaidi ya watu milioni 10 - hiyo ni nusu ya wakazi wa Congo wakati huo - walikufa kutokana na ukatili huo.

Serikali ya Ubelgiji ilichukua mamlaka mwaka wa 1908, na ikajulikana kama Congo ya Ubelgiji.

Congo ilipata uhuru mnamo Juni 30, 1960, na kupitisha jina la ‘’Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.’’

Hata hivyo, mwaka wa 1971, kiongozi wake Mobutu Sese Seko alibadilisha jina la nchi na kuwa Jamhuri ya Zaire - neno linalotokana na lugha ya kienyeji ya Kikongo - ikimaanisha 'Mto unaomeza mito mingine'.

Alipofariki mwaka 1997, jina lilibadilishwa na kuwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).

Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo mara nyingi huitwa Congo-Kinshasa ili kuitofautisha na Jamhuri ya Congo, ambayo mara nyingi hujulikana kama Kongo-Brazzaville.

Felix Tshisekedi ndiye Rais wa sasa wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo. Aliingia mamlakani mwaka wa 2019 na anahudumu kwa muhula wake wa pili baada ya kuchaguliwa tena Desemba 2023. Congo Kinshasa au DRC ndio ilikuwa ikiitwa Zaire toka 1971 hadi 1997 jina hilo liliitwa na Mobutu Sese Seko.

Jamhuri ya Congo (Kongo-Brazzaville)

Wakati Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) ilitawaliwa na Ubelgiji, Jamhuri ya Congo (Congo-Brazzaville) ilitawaliwa na Ufaransa kuanzia miaka ya 1880 na wakoloni waliitaja Brazzaville kuwa mji mkuu wake.

Wafaransa, ambao walijikita katika kuajiri wafanyakazi na kuchimba malighafi, waliwalazimisha Waafrika kujenga miundombinu ili kusaidia uchumi wa kikoloni.

Kwa mfano, inakadiriwa kuwa kati ya Waafrika 15,000 na 20,000 walikufa wakati wa ujenzi wa Reli ya Kongo-Ocean kati ya 1921 na 1934.

Congo-Brazzaville ilipata uhuru mnamo Agosti 15, 1960 na kupitisha jina la "Jamhuri ya Congo," ambayo imebaki nayo hadi leo.

Rais wa sasa wa Jamhuri ya Congo (Congo-Brazzaville) ni Denis Sassou Nguesso aliyeingia madarakani mwaka 1997.
 
UTOFAUTI WA CONGO NA CONGO.

Kongo ya Brazzaville na Congo Kinshasa ni majirani wanaohusiana kihistoria na kijiografia.

Kongo ya Brazzaville:
1. Jina rasmi: Jamhuri ya Kongo (Republic of Congo).
2. Mji mkuu: Brazzaville.
3. Rais: Rais wa sasa ni Denis Sassou Nguesso, ambaye amekuwa madarakani kwa vipindi viwili tofauti: 1979–1992 na tangu 1997 hadi sasa.
4. Historia: Jamhuri ya Kongo ilipata uhuru wake kutoka kwa Ufaransa tarehe 15 Agosti 1960.

Congo Kinshasa:
1. Jina rasmi: Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (Democratic Republic of the Congo).
2. Mji mkuu: Kinshasa.
3. Rais: Rais wa sasa ni Félix Tshisekedi, aliyeingia madarakani mwaka 2019.
4. Historia: Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ilipata uhuru wake kutoka kwa Ubelgiji tarehe 30 Juni 1960.

Uhusiano:
1. Kihistoria: Zote zilikuwa koloni za Ulaya; Kongo-Brazzaville ya Ufaransa na Congo-Kinshasa ya Ubelgiji.
2. Kijiografia: Miji mikuu ya Brazzaville na Kinshasa inatenganishwa na Mto Kongo na ni karibu sana kwa umbali.
3. Kiutamaduni: Wana utamaduni na lugha zinazofanana, kama vile Kifaransa na lugha za kienyeji kama Kikongo.
4. Kisiasa na Kiuchumi: Zote mbili zina historia ya migogoro ya kisiasa na kiuchumi, lakini zinaendelea kuwa na ushirikiano wa kibiashara na kidiplomasia.
 
Back
Top